Thursday, June 7, 2012
Riwaya mpya ya Kiswahili
UTANDAWAZI AU UTANDAWIZI?
JINSI LUGHA YA RIWAYA MPYA YA KISWAHILI INAVYODAI
Said A.M. Khamis
1.0 Utangulizi
Kuzuka kwa riwaya mpya ya Kiswahili katika miaka ya 1990 kunaelezwa kwa viwango
mbalimbali na wahakiki kama vile Wamitila (1991, 1997), Gromov (1998, 2004),
Khamis (1999, 2001, 2003, 2004), Bertoncini (2002), Topan (2002), King’ei (2002),
Dittemer (2002/2003) na Rettová (2004). Hapa, hatuna nafasi ya kurejelea tabia za
‘kimaumbo’, ‘kimiundo’ na ‘kimaudhui’ zinazoitofautisha riwaya hii ya Kiswahili na
nyingine, ila tutajishughulisha na kipengele kimoja tu cha msingi, nacho ni kipengele cha
lugha kama alama mojawapo ya mtindo1 au mwelekeo wa riwaya hii – lugha katika
uhusiano wake na utandawazi au utandawizi.
Katika makala haya tunatilia mkazo kwamba aina ya lugha inayotumika katika
kazi fulani ya fasihi huathiriwa na nini kinachotokea katika jamii yenyewe ambamo
mwandishi huchota fikira, maudhui, falsafa, itikadi, jazanda, mitindo, maumbo na
miundo-lugha –hasa inapokuwa jamii yenyewe imo katika kasi ya mabadiliko makubwa
kama ambavyo tumekuwa tukishuhudia kuanzia wakati riwaya hii ilipoibuka katika
miaka ya 1990 hadi leo.
2.0 Riwaya Mpya na Utandawazi
Riwaya ya Kiswahili tunayoizungumzia imezaliwa mwanzoni mwa miaka ya 1990, muda
mfupi tu baada ya neno utandawazi kuingia masikioni na kuzama akilini mwetu kuanzia
miaka 1980. Utandawazi ni neno dhahania mno, lenye maana nyingi zenye utata
kutegemea msisitizo wa anayelitumia. Pamoja na tofauti za maana na matumizi ya neno
hili, wataalamu wanakubaliana kwamba ni neno linaloelezea mfungamano na uhusiano
uliojitokeza katika miaka 30 iliyopita; hasa katika biashara na uchumi, lakini pia katika
utamaduni, miongoni mwa jamii tofauti za dunia. Mfungamano na uhusianao huu
unatofautishwa na mfungamano na mahusiano mengine ya aina hii yaliyojitokeza hapo
awali, kwa sababu utandawazi umepata kasi kubwa ya kuwekeza mitaji na kuvuna
bamvua la faida kiuchumi na kiutamaduni; ukisaidiwa na maendeleo makubwa ya
kiteknolojia yaliyopatikana karibuni, hasa ya vyombo vya mawasiliano ambavyo
vimefupisha au kuondoa vikwazo vya masafa na wakati (Jauch 2001, Offiong 2001).
Kiutamaduni, utandawazi unahusishwa na kuenea kwa tamaduni za ki-Magharibi kwa
njia ya kibiashara (k.m vinywaji vya Coca Cola, bia na pombe kali ambazo hapo zamani
zilikuwa hazijulikani au zilijulikana kwa watu wachache tu wa Dunia ya Tatu na vyakula
vya Kentucky na Mcdonald) au mtiririko wa muziki na taswira kupitia video, televisheni,
mitandao ya kompyuta na simu, CD, DVD na VCD. Lakini kwa hakika si sahihi
kuuchukulia utandawazi kijuujuu tu, au jinsi unavyofasiliwa na watetezi wake. Kwa
hivyo, ipo haja hapa kuelezea, ingawa kwa ufupi, asili ya kuibuka kwake.
Historia ya utandawazi haiwezi kuepushwa na misingi ya mikakati ya G7, Benki
ya Dunia, IMF na WTO, vyombo vinavyosimamiwa, kuimarishwa na kuendelezwa na
itikadi ya uliberali-mpya2 (Jauch 2001; 3-15; Offiong, 2001: 1-19). Kwa kweli,
1 Tunapenda kukumbusha kwamba hii ni maana moja tu ya mtindo – yaani mbinu ya pamoja inayotofautisha kundi la
2 Tafsiri ya ’neo-liberalism’
kinadharia, mfungamano na uhusiano huu wa utandawazi unafasiliwa kwa namna tofauti
baina ya kambi mbili. Kambi ya kwanza inauchukulia utandawazi kuwa ni ‘baraka’ kwa
nchi zote duniani, kwa sababu hatimaye utaboresha maisha ya watu wote duniani kote
(Ruigrok & Van Tulder 1995:169). Kambi hii inadai kwamba utandawazi una faida
kubwa hasa kwa nchi zinazoendelea3, na kwamba kufungua milango ya biashara, masoko
huria ya bidhaa na kuufanya utamaduni wa taifa moja ukutane uso kwa uso na utamaduni
wa mataifa mengine (sifa moja kubwa ya utandawazi), kunaleta fanaka kila pahala
(Jauch, keshatajwa: 3).
Kambi ya pili, ikitumia ithibati jarabati, inakanusha kabisa uhalali wa madai ya
kambi ya kwanza, kwa kusema kwamba utandawazi si dhana mpya kamwe, bali ni upeo
wa dhana kongwe yenye sifa mpya ya kutumia maendeleo makubwa yaliyopatikana
kiteknolojia, kunyonya, kwa mapana na marefu, utajiri wa dunia na kuwaacha watu wa
nchi masikini kuwa masikini zaidi kuliko walivyokuwa zamani. Na si kuwaacha masikini
zaidi tu, bali pia kuchafua uchumi, tamaduni, mazingira na maisha yao vibayavibaya,
hadi kufikia nchi hizo kudharauliwa na kuonekana si lolote si chochote katika fikra ya
dunia hivi leo. Mabadiliko haya, kwa sehemu kubwa, yanatokana na upeo wa matatizo ya
kiuchumi ya kimataifa yaliyotokea mwanzoni mwa miaka ya 1970, ambayo
yalisababishwa na maslahi ya kibiashara na utashi wa mataifa makubwa yanayolenga kila
siku kupata faida kubwa kupita kiasi (Murray 2000:7-8; ILRIG 1998).
Jumla ya riwaya za Kiswahili tunazoita mpya ni zile za Euphrase Kezilahabi za
Nagona (1990) na Mzingile (1990), riwaya moja ya Katama Mkangi ya Walenisi (1995),
riwaya ya W. E. Mkufya ya Ziraili na Zirani (1999), riwaya moja ya Mohamed ya Babu
Alipofufuka (2001) na miswada yake miwili4 ya Dunia Yao na Mkamandume, riwaya
moja ya Wamitila ya Bina-Adamu (2002) na, kwa namna na kiwango fulani, riwaya ya
Chachage ya Makuadi wa Soko Huria (2002).
Sifa moja kubwa ya kimaudhui, miongoni mwa sifa kadha za riwaya hii, ni ile ya
kushughulikia kwa kina matatizo ambayo yanaukabili ulimwengu wetu leo. Kwa namna
nyingine tunaweza kusema, ingawa bado riwaya hii inajishughulisha kwa kiwango fulani,
na matatizo ya ndani ya nchi na jamii husika, kwa kiasi kikubwa imekiuka mipaka ya
kitaifa na kieneo. Kwenye jalada la nyuma la Bina-Adamu, tunaambiwa wazi kwamba…
[n]i riwaya inayotumia sitiari ya kijiji kuangalia hali ya mataifa ya ulimwengu. Katika
kuhitimisha makala yake Postmodernistic Elements in Recent Kiswahili Novels, Gromov
(2004:13) anatuambia:
[t]unaweza kusema kwamba fasihi ya Kiswahili inaendelea kuchukua dhima ya
uchunguzi wa jamii –lakini, huku ikibeba silaha mpya za njia ya utunzi na fikra za
majadiliano, inajishughulisha na matatizo mapya, na inachunguza, si jamii ya Afrika
Mashariki tu, bali dunia yote kubwa (na) pumbavu, isiyoishika tena, lakini ndiyo pekee
tuliyonayo– dunia yetu ya leo ...
(tafsiri yangu).
3 Sina hakika kwamba neno hili tunaweza kuendelea kulitumia kurejelea nchi zetu za Kiafrika, lakini nitalitumia kwa
kukosa neno linalofaa zaidi.
4 Dunia Yao ni mswada uliopelekwa Jomo Kenyatta Foundation tangu 2001 na kukubaliwa kuchapishwa lakini
mwandishi aliuondoa huko, kwa kuchelewa kuchapishwa, akaupeleka OUP ambako nako umekaa tangu Julai, 2004.
Ms wa Mkamandume ulimalizwa kuandikwa mwaka 2004 na bado haujawasilishwa kwa watoa vitabu wowote.
Ingawa riwaya hii mpya, kama tulivyosema, inajishughulisha na mada mbalimbali za
kimaudhui kuhusu matatizo yanayoikabili dunia yetu ya leo –hapa tumechagua
kuzungumzia, kwa mujibu wa maoni yetu, tatizo kubwa na sugu kabisa la utandawazi–
tatizo ambalo riwaya kama Nagona, Mzingile, Babu Alipofufuka, Dunia Yao, Bina-
Adamu na Mkamandume, zinalijadili waziwazi. Kwa mfano, katika kuthibitisha namna
gani dhamira ya utandawazi inavyotawala katika Bina-Adamu, Gromov (2004:8), akiteua
kwa uangalifu lugha na picha zinazoelezea dhana ya utandawazi, anatambia hivi:
Wakati wa safari yake ndefu, mbabe, akisaidiwa na sauti ya ajabu ya mwanamke
mwenye sifa zisizo za kibinamu anayeitwa Hanna, anazuru Ulaya ambayo ‘inaishi jana’,
Asia ya viwanda ambayo ‘inaishi kwa matumaini’ na Afrika, ambayo ‘inaishi mwishoni
mwa kijiji cha utandawazi na imeharibiwaharibiwa na njaa na vita. Anapokuwa njiani,
kila pahala anakutana na mambo yanayoonekana hayana mantiki, mambo ambayo
hayaelezeki yanayofanywa na P. P mwenye miujiza –Ulaya P. P ameushinda ufashisti,
lakini bado unaishi imara miongoni mwa wafuasi wake. Huko Asia ametupa bomu la
Atomiki Hiroshima. Afrika, akitumia jiwe, amevigonga vichwa vya wanasiasa kuvitoa
akili. Huko Urusi, ambako P. P anazuru kwa muda mfupi, hatuambii anafanya nini kwa
vile anamwogopa Stalin. P. P anaiuza Afrika kwa watalii wa kigeni, anaharibu bahari
kwa mafuta na mabaki machafu ya ‘radioactive’: Mwishoni mwa safari yake mbabe
anaigundua Amerika –Bustani ya Adeni ya pili, ambamo wakazi wake, mapapa wa
biashara za kimataifa, wanaishi (vizuri) kutokana na umasikini wa Nchi za Dunia ya
Tatu, wakidai kwamba wanaishi leo na tena wanaishi katika uhalisia wa mambo ...
(tafsiri yangu)
Msomaji anaposoma lugha hii, anaona moja kwa moja kwamba huu ni mfano mmoja wa
waandishi wa riwaya hii ambao wanapinga kwamba utandwazi una neema yoyote ile kwa
nchi za Dunia ya Tatu. Na kusema kweli, hawaishii hapo tu. Wanaonyesha hasira zao
kwa kile ambacho wao wanaona ni ujinga wa viongozi au serikali zetu kukubali kiholela
kuihonga nchi kwa mataifa makubwa. Itakuwaje mataifa G7 ambayo yalitukandamiza
kwa kila hali wakati wa ukoloni ndio leo yawe yanayotutakia mema? Itakuwaje vyombo
kama Benki ya Dunia, IMF na WTO ambavyo vimekuwa vikitoa mikopo kwa masharti
magumu mpaka kutunyang’anya uhuru wa kila kitu, viwe ni vyombo vya kutufikisha
pahala pema? Itakuwaje itikadi ya uliberali-mpya iwe ndiyo itikadi ya kusafiria kwa nchi
za kimasikini? Itakuwaje nchi zetu ziweze kuingia katika mashindano ya kibiashara na
USA, Ulaya ya Magharibi, Japani, Australia na Korea ya Kusini? Vipi suala la ndizi za
Jamaika? Je, huu haukuwa mfano wa kutosha wa kutufumbua macho? Wakulima wetu
wanawezaje kushindana katika uzalishaji na uuzaji wa bidhaa na wakulima wa mataifa
makubwa yanayopata fidia kubwa kutoka serikali zao? Hivi historia nzima ya udhalimu
wa ukoloni na ukoloni mamboleo, haijawa funzo la kutufanya tushituke na kuuangalia
uhusiano wetu na dunia upya na kwa makini zaidi? Kwa mujibu wa waandishi wa riwaya
hizi, kukubali kudanganyika kirahisi na mambo haya, kumesababisha kuporomoka
vibaya sana kwa nchi zetu katika sekta zake zote, ingawa takwimu za ukuaji wa uchumi
zinazotolewa na wakubwa, zinawekwa juu. Hii ndiyo sababu mwandishi mmoja kati yao,
Wamitila (keshatajwa: 85, 87, 155), ametumia neno utandawizi, badala ya utandawazi –
kijiji cha Global Villain, global pillage.
3.0 Matumizi ya Lugha katika Riwaya Mpya
Kwa ujumla, lugha ya aina hii ya riwaya mpya ya Kiswahili ina tabia tofauti na lugha ya
aina nyingine za riwaya ya Kiswahili tangulizi ambazo zimekita kwenye uhalisia mkavu.
Sifa ya mwanzo na ambayo ni ya msingi, ni ile ya usasabaadaye, ambao, kama mtindo
fulani wa fasihi na sanaa kwa ujumla, unakwenda sambamba na utandawazi au ubepari
mpevu, kuonyesha mkinzano mkubwa uliomo ndani ya mfumo wake. Usasabaadaye ni
mfumo ambao huvunja kanuni zote za kijadi, kaida na namna ya kutumia lugha kisanaa.
Sifa ya pili ni ya utouzowefu5 neno lililoanzishwa na shule ya urasimukanuni lenye
kubeba maana na kazi maalumu katika fasihi –kazi ya kuichangamsha na kuitia lugha
uvuguvugu ili inonekane mpya au ngeni kuliko ilivyokuwa, lengo kubwa likiwa
kubadilisha mtazamo wa msomaji kwa kumwonesha ujumi wa lugha ambao utachukua
makini ya msomaji, kumvuta kisanaa na kumfanya afikiri zaidi. Kwa mfano Mohamed
katika Babu Alipofufuka (2001:13) anacheza na lugha kwa namna ifuatayo:
[I]nasemakana Delpiero karibuni amemeza eneo zima la ardhi la pahala fulani tumboni
mwake. Wavuvi waliposimama kidete kupuliza cheche zao za uchungu, K alikuja juu
kuwaambia wastarehee neema zao ...
Sifa ya tatu ambayo pia inashikana na sifa ya mwanzo na ya pili ni ile ya
mvutogubi6. Neno hili linasimamia mjazo wa jazanda zenye fumbo, nguvu na mapigo ya
kimuziki ambayo mara kadha huonekana ni muhimu zaidi kuliko maana – ingawa katika
riwaya hii maana bado inabaki kuimarishwa. Hapa kwa mfano, tuna mchezo wa
mvutogubi kutokana na riwaya ya Wamitila, Bina-Adamu (2002: 40):
[S]ikujua kama nilikuwa nikitembea kuelekea jana au kwenda kesho au labda nilikuwa
leo. Labda nilikuwa kote wakati mmoja ...
Sifa ya nne, ni ile ya mchanganyo ndimi, hasa kwa sababu riwaya hii mara nyingi
husomba na kujaza kila kitu katika matini yake: historia (‘Vita vya Fyura’ – Bina-Adamu
uk. 34), uchumi (‘Nchi nyingi katika ulimwengu wa tatu zilipata pigo kubwa la njaa na
mamilioni ya watu walikufa. Migogoro mingi ya kiuchumi iliendelea kuisakama dunia’ –
Nagona uk. 18), siasa (‘Dunia yao ndivyo ilivyo; si hii yetu: Kwao taka husafishwa kwa
taka; uungwana husafishwa na utumwa –madhali tu K anaramba kamasi tamu za pua...’ –
Babu Alipofufuka uk. 10), utamaduni (‘Tupige darubini hivi vitu tunavyovikimbilia
kutoka nje. Hizi video na filamu ni propaganda isiyokuwa ya moja kwa moja.
Zinatumiwa kusambaza na kutangaza taswira maalumu za utamaduni mmoja tu...’ Bina-
Adamu uk. 40), muziki (‘Nilipoingia ndani nilitia CD ya wimbo wa taarab wa Mohamed
Ilyas: La Hasha!’ –Dunia Yao uk.87). Kisaikolojia, riwaya zote zinaonyeshwa akili za
wananchi kufunikwa na utandu.
Kwa matatizo ya utandawazi na mengine yanayoibua matatizo ya kisaikolojia na
kisosholojia, mkondo mzima unaomchukua mwanadamu kubadilika na kuwa mnyama,
unachunguzwa katika riwaya hizi kupitia kile ambacho tungeliweza kukiita sosiolojia ya
riwaya. Aidha mna mchanganyiko wa visaasili, migani na harafa.
5 Tasiri ya Defamiliarisation ambayo ni tafsiri ya ’ostranenie’, neno la Kirusi lililoanzishwa na Viktor
Shklovsky
6 Tafsiri ya Hermetic
3.1 Lugha na Usasabaadaye
Kwa vyovyote vile, chochote kile kinachohusiana na kilichomo ndani ya fasihi na jinsi
kinavyowasilishwa katika kazi hiyo, lazima kihusishwe na matumizi mbalimbali ya
lugha. Makala haya yanatambua ukweli kwamba kile ambacho, kwa mfano, kinaitenga
lugha ya sayansi na fasihi ni jinsi lugha inavyojitokeza tofauti kimaumbo, kimsamiati na
kimuundo katika nyanja hizi mbili. Ukweli huu umo pia katika namna lugha za ushairi na
nathari, uhalisia na fantasia, usasa ulioanza baada ya Vita vya Kwanza vya Dunia; na
usasabaadaye, ulioanza baada ya Vita vya Pili ya Dunia na kwenda mbele zaidi kuigeuza
riwaya ya uhalisia jinsi ilivyokuwa kabla ya kuzuka kwa usasa huko Ulaya.
Usasabaadaye, kama njia moja ya kubuni kazi za fasihi, ulianza mapema tokea
miaka 1950, baada ya kuporomoka kwa uhalisia na usasa. Lakini ni katika miaka ya
1980 ndipo usasabaadaye ulipopata upana wa matumizi katika nyanja za falsafa na
utamaduni na pia katika fasihi na uhakiki wa kifasihi (Gromov 2004:1). Lengo kuu la
usasabaadaye, kinyume na uhalisia na usasa, ni kuonyesha kutoweza kwa mwanadamu
kuufahamu ulimwengu, kwa sababu urazini wa mwanadamu hauwezi tena, katika hatua
hii, kuutambua utata wa ulimwengu. Kile kinachowezekana labda ni kuchunguza picha
au alama za vitu. Hii ni kusema kwamba mwanadamu haufahamu ulimwengu wake kwa
sababu tu umekuwa ni ‘uwanja wa fujo’, bali pia kwa sababu ni kama matini tu; yaani
mlimbikizo usiokuwa na mwisho wa alama zinazobuniwa kutokana na urazini wa
mwanadamu. Kwa hivyo, uzoefu wa mwanadamu, historia yake, utamaduni wake –kila
kitu ni mkondo wa alama, ambamo zile zilizo tata hutokana na zile sahili zilizokuwepo
hapo awali.
Hapa tutaitazama lugha ya riwaya mpya katika ugo huo. Lakini kabla hatujafanya
hivyo, yafaa tukawazindua wasomaji wetu juu ya jambo moja ambalo Gromov
(keshatajwa) analieleza na ambalo ni la kipekee katika riwaya hii mpya ukilinganisha na
usasabaadaye katika fasihi za lugha na tamaduni nyingine. Jambo hili linahusiana na
namna waandishi wa riwaya hii mpya wanavyobaki kung’ang’ania tamaa na kutukuza
utu na ubinadamu. Katika hitimisho lake Gromov (keshatajwa: 12-13) anatwambia ...
[l]azima tugundue kwamba kuna tofauti kubwa baina ya umahiri wa usasabaadaye wa
nchi za ki-Magharaibi na ule wa jamaa zao wa Afrika Mashariki, Kiswahili
kinakozungumzwa. Waandishi wa Kiswahili katika kuvutika na usasabaadaye wana
mtazamo na msimamo wa pekee kuhusu maana na umuhimu wa ujumi ukilinganisha na
ule wa wanausasabaadaye wa ki-Magharibi –wanausasabaadaye wa Kiswahili wana
mtazamo mkali juu ya kuvunjiwa thamani dunia. Katika mtazamo wao mkali, waandishi
wa riwaya mpya ya Kiswahili, utu na mapenzi vinatetewa kama tunavyosoma katika
Bina-Adamu, pale mhusika mkuu Binadamu Msafiri anapoonywa kuutunza mkoba
aliopewa na babu na kuambiwa ... [U]tunze huu, ndani mna utu, mapenzi na kiini cha
kuwako kwako. Mkoba huu utakufaa sana siku zijazo: Usiudharau kwa sura yake;
mwacha asili ni mtumwa ...
Makala haya yanakubaliana sana na Gromov kuhusiana na ugunduzi huu muhimu wa
suala la utu na mapenzi katika riwaya mpya ya Kiswahili na waandishi wake. Lengo
mojawapo la makala haya ni kudhihirisha hivyo.
3.2 Lugha ya Uhakiki na Mkemeo wa Utandawazi
Waandishi wa riwaya mpya ya Kiswahili katika uhakiki wao wa siasa na mwenendo wa
jamii, wanataja wazi kwamba umefika wakati sasa Mwafrika ajilaumu mwenyewe juu ya
balaa lote linalomkuta; na la kulaumiwa zaidi, hasa, ni taratibu za uongozi zitumikazo
katika Afrika. Kuhusu suala hili Mohamed, katika Babu Alipofufuka (uk.10) anatuambia:
[S]iku hizi K, kinyinginya changu, anaweza kuketi meza moja na watu ambao miaka
michache iliyopita ilikuwa mwiko kukaa nao. Mazimwi, aliwaita. Akatangaza vita nao
kwa kusaidiwa na nyuki...
Kwa waandishi hawa, kuwakaribisha mabeberu, bila au kwa viwango vilivyopo vya
malipo ya uwekezaji ili kuchukua rasilimali za nchi zetu na kutumia jasho la watu wetu,
ni ujinga usiokuwa na mfano. Mohamed katika Babu Alipofufuka (uk.13-14) akiwaelezea
wahusika wake wa kigeni anathibitisha tena ujinga huu kwa maneno haya:
[I]nasemekana Delpiero karibuni amemeza eneo zima la ardhi la pahala fulani tumboni
mwake. Wavuvi waliposimama kidete kupuliza cheche zao za uchungu, K alikuja juu
kuwaambia wastarehee neema zao... Miyazawa aliyetoka kwao juzijuzi na kuwa
mwenyeji kuliko wenyeji, haonekani na mtu yeyote kuwa na kazi ya maana nchini humo
ila sifa zake za mkonowazi... Naye Von Heim, ana nia kubwa ya kusaidia kumfufua maiti
kwa kummiminia bia kutokana na tangi lake kubwa... Tena kulikuwa na Di Livio ambaye
kaja huku kucheza kamari. Halali mchana wala usiku; yumo mbioni vilabuni, mabasini,
mandarini, hotelini...
Kusema kweli, ujinga wetu hauko katika kukubali kuibiwa tu rasilimali zetu, bali pia
kukubali kupokea vibovu na vichafu kwa thamani kubwa. Wamitila (keshatajwa)
anaiendeleza fikra hii kwa maneno haya:
“Hiki ni kiwanda.”
“Cha nini?”
“Reconditioned cars.”
“Mnazitumia?”
“Ahh, deki masen! Haiwezekani asilani. Sheria zetu zinakataza matumizi ya
magari hayo.”
“Basi mnayetengenezea nini?”
“Kuna soko kubwa huko upande wa chini. Huko ndiko tunakotupa
tusivyovihitaji.”
“Mnavitupa ehh?”
“Mmm, ni hivi tuseme, wanakubali wenyewe; ...”
Kauli kali kabisa ya uhakiki na mkemeo wa waandishi hawa kuhusu ujinga wetu
unapatikana katika mswada wa riwaya ya Mohamed, Dunia Yao (38), kauli ambayo
inathibitisha jinsi gani tulivyotoa nafasi kutawaliwa, kwa kuogopa kutopata ruzuku au
kwa kutarajia uokovu kutokana na utandawazi:
Wamechukua kila kitu: niliendelea; wao wamekuwa ndio wafikiri wetu, wasemaji wetu,
wanaohisi kwa ajili yetu, wanaoona njaa na kiu zetu, walimu, madakitari, wanafalsafa,
wanauchumi, mashehe, mapadre, walinzi wetu ... kwa ujumla waendesha maisha yetu
yote; sehemu ya viwiliwili na akili zetu ... kwa ufupi wao ni kila kitu! Sisi wengine ni
mapipa matupu. Hatuna rojo la uhai: Hatuna supu ya maisha wala nyama ya ubinadamu
wetu. Hatuna sehemu ya utu. Hatuna rai. Hatuna maoni. Hatuna chetu. Hatuwezi kufikiri
kama wao au zaidi ya wao. Hatutarajiwi kusema. Hatutarajiwi kushiriki hata mambo
yanayohusu nafsi zetu. Chambilecho Fowles... Kuna mtazamo fulani wa kisasa katika
dunia yetu kwamba falsafa waachiwe wanafalsafa, elimujamii iwe bahari ya kuogelewa
na wanaelimujamii na kifo kwa maiti.
Lugha hii ya uhakiki na mkemeo kwa utandawazi inakita katika kauli, picha na
jazanda zinazojenga kejeli au tashititi. Katika matumizi ya lugha ya namna hii waandishi
hawa wanatoa dalili ya ujinga wa jamii na uongozi wao na uchungu walionao kwa ujinga
huo unaotendeka –dalili ambazo zinaweza kupewa tafsiri tofauti miongoni mwa
wasomaji. Kwa mfano, haifahamiki nani kaelekezwa nalo dondoo hilo hapo juu: utawala
wetu wa ndani? Makuadi wa soko huria? Ukoloni mamboleo? Wakoloni mamboleo
wenyewe? Utandawazi au waasisi wa utandawazi na vyombo vyao? Utandawizi ambao
unajidhihirisha katika mshuko wa kiwango cha chini kabisa katika heshima ya dunia?
Uelezaji huu unalingana na unakwenda sanjari na utata na mkinzano wa mambo
mengi jinsi yanavyokwenda katika dunia yetu ya leo. Fikiria utata na mkinzano wa
utawala au uongozi wetu wa ndani na haki za raia zinazovunjwa ovyoovyo. Fikiria
ukoloni mamboleo na utandawazi wenyewe unavyovunjavunja kila kitu na jinsi matokeo
yake yanavyoafikiana sana na matumizi ya lugha katika riwaya hii.
3.3. Ujengaji Fantasia na Uhalisia Mazingaombwe
Sifa iliyo dhahiri sana katika riwaya hii ni namna gani lugha inavyotumiwa kujenga kwa
makusudi fantasia na uhalisia mazingaombwe. Katika makala haya tunatofautisha
fantasia na uhalisia kwa sababu fantasia ni dhana inayoelezea njia ya kutumia lugha kwa
kutia chumvi mno, hadi kufikia kuvuka mstari wa uhalisia na mantiki. Kwa maneno
mengine, fantasia ni dhana pana inayohusiana na chochote kinachoelezewa kwa kutiwa
chumvi na kusimama nje ya uhalisia na mantiki. Uhalisia mazingaombwe ni aina fulani
ya fantasia, lakini ni mbinu inayozileta dunia mbili pamoja za ‘ukale’ na ‘usasa’ –ukale
wenye misingi ya mazingaombwe au ukweli ambao hauwezi kuelezeka katika mantiki ya
nchi za Ulaya. Na usasa unaojaa taathira za kitamaduni, sayansi na teknolojia iliyoletwa
na wakati wa ukoloni na wakati baada ya ukoloni.
Tunaweza kusema kwamba Shaaban Robert ni mwanzilishi wa riwaya ya fantasia
katika fasihi ya Kiswahili, hasa katika Kusadikika (1951), Adili na Nduguze (1952) na
Kufikirika (1967). Lakini ingawa riwaya hizi zina uhalisia wa aina fulani, fantasia yake
ni tofauti na ile ya riwaya mpya, kwa vile zimejikita mno katika ubunifudhanifu wa kila
kipengele chake: ‘simulizi’, ‘hadithi’, ‘uhusika’, ‘mandhari’ na hata ‘uhalisia’ wa baadhi
ya miketo7 ya matini yake. Fantasia ya riwaya mpya ni ya kuuelezea ukweli kama ulivyo
hivi sasa na kwa hivyo uko karibu na kinachotokea katika mandhari, karibu na simulizi
na wahusika wa riwaya yenyewe. Ingawa huu ni uhalisia mazingaombwe una mnato zaidi
kuliko fantasia ya Shaaban Robert.
Fantasia na uhalisia mazingaombwe ni pumzi za riwaya mpya. Huwezi kusoma
ukurasa mmoja au hata pengine aya moja bila ya kujikuta unatoka katika uhalisia na
kuingia katika mazingaombwe au kutoka mazingaombwe na kuingia katika uhalisia.
Mpaka baina ya matukio au dunia hizi mbili ni mfinyu mno kiasi kwamba ni sawa na
7 Tafsiri ya Chunks
kusema haupo. Mbinu hii imetawala katika riwaya zote za mwelekeo huu –mbinu ya
uhalisia usio uhalisia, mazingaombwe yasiyo mazingaombwe, fantasia isiyo fantasia.
Katika Nagona kuna mto unaonguruma usioonekana, ukohozi wa watu
wasiokuwepo, miti inayocheka, hali ya mhusika kuchapwa na watu usiowaona, ukimya
unaokatwa ghafla na sauti za watu wanaosoma wasioonekana (yote katika uk. 1 tu), maiti
aliyefumbatwa katika kiza ambaye anashika Biblia mkono mmoja na Koran mkono
mwingine, paka wa ajabu anayetarajiwa kuwa mlinzi wa mauti (uk.2-3), bustani yenye
maua meupe yanayoteleza na kutoa mwangaza, maua na matunda ambayo hayawezekani
kuvunwa (uk.13), kikundi cha wafu cha wanafalsafa mashuhuri, wanabiolojia,
wanasosiolojia na wanasaikolojia wanaofufuka ... (uk.15).
Katika Babu Alipofufuka kuna dhana nzima ya fikira kwamba hatufi, tunapita tu
katika dunia nyingine ya kutoonekana tukiwa mizuka, dhana nzima ya ndoto anayoiota
binadamu katika dunia yetu ya leo, ndoto ambamo ndani yake binadamu anajiona hana
hakika kama yupo au hayupo, anaishi au amekufa. Pia katika riwaya hii kuna miujiza ya
aliye hai kuweza kujiua na kujifufua tena au kujigeuza mchwa na kurejea tena katika
umbo la kibinaadamu au kuzama chini ya ardhi na kuibuka baharini na tena ghafla
kukanyaga nchi kavu.
Katika Bina-Adamu kuna miujiza ya kutumika chakula na kinywaji kisichokwisha
na ambacho kinashibisha mara moja. Au ya mhusika kuweza kusafiri dunia nzima
kifikira au ndoto, kupitia nchi kavu na mtoni na baharini. Kuna hali ya mtu mzima kurudi
utoto kimaumbile. Mna viumbe wa miujiza kama lile jitu lenye miguu mirefu kupita kiasi
ambalo linaitwa beberu au UMERO-JAPA. Au aina ya kiumbe mwingine anayeitwa
Wotan, Mungu wa vita na mfalme wa mashujaa. Au mahuntha watatu ambao
wanatafutwa lakini hawaonekani kwa sababu ni viumbe wa miujiza. Kuna P.P (Peter Pan
/Yanguis??) mwenyewe ambaye ana miujiza ya kinanga8 na kuzongwa na visaasili
ambaye pia anatafutwa na mhusika mkuu ili iwe ni sababu ya kukikomboa kijiji
kilichotengwa mno duniani. Viumbe wengine wa miujiza ni wale watu waliofufuliwa,
akina Fyura (yaani Fuehrer, lakabu aliyopewa kiongozi wa kiimla Adolf Hitler), Dkt.
Joseph Mengele, Hiro (Hirohito, aliyekuwa mfalme wa Japan), Osagyefo (yaani
marehemu Kwame Nkrumah), Churchill na Stalin. Mwalimu au Mussa anayeishi vileleni
mwa miti na ambaye anapenda sifa na kuimbiwa nyimbo (labda marehemu mwalimu
Nyerere).
Katika Ziraili na Zirani kuna mpaka mdogo sana wa maisha ya duniani na
mbinguni. Kuna mchanganyiko wa watu, malaika na Uungu. Kuna roho kusimama na
kusema au ufufuzi wa watu wanaosema na majini, mashetani na malaika. Pia katika
riwaya hii maisha ya mbinguni yanachorwa kisitiari na kufananishwa na maisha yetu
tuliyonayo leo: maisha yaliyojaa suitafahamu za kiitikadi za kidini na siasa, uonevu,
mabavu, unyonyaji, uongo, unafiki, ufisadi, njama, ugomvi na vita. Mlinganisho huu ni
wa uhusiano wa karibu mno mpaka msomaji anajiuliza kama mwandishi anazungumza
kwa njia ya ishara na fumbo, ahera au dunia tunayoishi leo.
Katika Dunia Yao, mazingaombwe yamo katika ile hali ya mhusika kuikimbia
nafsi yake, familia yake, marafiki, majirani na jamii kwa jumla; ile hali ya mporomoko
wake unaomrusha akili na kumfanya aishi kwenye chumba kidogo mfano wa jela
ambamo anazurura katika dunia pana bila ya kuzurura. Anamozurura katika ndoto.
Katika dunia hii mhusika mkuu anapanga udugu na kompyuta, mtu-mashine pekee
8 Tafsiri ya Epic
aliyebaki katika maisha yake anayeweza kumwamini, kuzungumza naye, kushauriana
naye, kumtumia kama kiwango cha kuandikia historia na hadithi yake na hadithi za watu
wengine na kiwambo cha kuweza kuzungumza na binti yake ambaye anaishi London
kama mkimbizi-njaa. Kuna wahusika-picha wanaosimama kutoka katika albamu na kuwa
viumbe vyenye ngozi, nyama, damu na mifupa –viumbe vyenye urazini kamili. Ndani ya
riwaya hii pia kuna mtoto mkombozi9 ambaye tokea siku yake ya kuja duniani
anaonyesha miujiza ya kusema, kula, kutembea na kutoa rai kama vile mtu mzima. Pia
katika riwaya hii kuna matambiko yanayohusishwa na Miungu ya Kiafrika kama ile ya
kosmolojia ya Waibo wa Nigeria.
Jambo muhimu hapa ni kukumbuka kwamba fantasia na uhalisia mazingaombwe
hayapo kwa ajili ya kuwepo tu au kwa ajili ya mchezo wa lugha na sanaa. Ni mbinu
muhimu ya kumfanya msomaji autupie jicho kali uhalisia mpya ambao una ukweli wa
aina nyingine kabisa, uhalisia wenye mkanganyo na utata. Ni mbinu ya kukemea kile
kinachoonekana na waandishi hawa kuwa ni utandawizi badala ya utandawazi. Ni mbinu
ya kuonyesha mporomoko wa kila kitu katika jamii zetu –uchumi, utamaduni, uhusiano
baina ya mtu na mtu, uhusiano wa raia, umakinifu wa ukoo na mtu binafsi kama
Mtanzania na Mkenya, utambulisho wa mtu binafsi ambao umesambaratika na kuteremka
chini kwa kiwango kikubwa mno, au kuporomoka kwa huduma za kijamii, kunajisika
kwa heshima ya Mwafrika, Mtanzania, Mkenya na mpopote-pale-alipo ulimwenguni.
Ushahidi mzuri wa fantasia na uhalisia mazingaombwe umo katika dondoo hili la
Mohamed katika Dunia Yao (uk.172-173) – dondoo ambalo linaelezea dhana ya
utandawazi katika picha za kimiujiza kabisa:
Sasa hivi ndiyo kile kitu kimeshakaribia. Karibu mno kuweza kutambulikana. Kitu gani?
Ilikuwa vigumu hata kubahatisha kukiagua au kukitaja kwa asahi. Kitu au jitu? Utata wa
jitukitu labda. Umbo lake limekas’mika nusu bin nusu, kushoto na kulia, katikati ya
jimwili lake. Pandikizi la jitukitu jinsi lilivyoumbika. Kushoto, linamemetuka anga la ki-
Ungu linaloumiza macho na kuogofya. Kushoto pia linachanua uzuri wa ajabu. Uzuri wa
kike ndani ya uzuri wa kiume. Uzuri unaokanganya. Sijapata kuona kiumbe duniani
chenye uzuri namna hii. Useme hao huru-l-ayen wa peponi watajikanao. Na kulia,
jimwili lake limekumbatiwa na giza zito la maangamizi ambalo kila mara lilikuwa
likiripuka moto kuunguza kila kitu kilichosimama kwenye njia yake. Lilikuwa likipita
kwa kasi ya umeme, lakini bado lilionekana lipo papo hapo daima – haliondoki! Linapiga
kasi katika njia yake inayojiandika yenyewe – mara Globalization mara Americanization.
Na lilipotimka lilitifua kila kitu katika kasi na mikiki yake. Kila kitu kilipojaribu
kufukuzana nalo, kilijikuta kinaachwa nyuma milioni ya kilomita. Likapita kwa kasi na
pepo zake za dhoruba likiripuka mandimi ya moto yaliyounguza na kukausha kila kitu:
watu, wanyama, barabara, majumba, miji, maji, hewa, pwani, bahari, nchi kavu, madini,
umeme, mafuta, hospitali, madawa, benki, viwanda, biashara, raslimali zote ... shule,
vyuo, desturi, mila, tamaduni na hata uhai, heshima na mustakabali wa watu – hata roho
zao. Lilipenya hata ndani ya nyumba na vibanda vya watu kusasambura na kupekua kila
kitu kukashifu na kufedhehi na kisha kuangamiza lilivyopenda. Liliingia humo na
kutawala na kuamrisha na kulazimisha mambo katika nyumba yake mwenyewe mtu ...
Ingawa huu si mkemeo kamili (labda ni maombolezo), bado lakini tunaona hasira za
mwandishi na kutokubaliana kwake na dhana ya utandawazi iliyoingia katika vichwa vya
9 Katika riwaya hii mpya ‘mkombozi’ ni neno muhimu sana linalorejelewa katika nyingi ya matini ya
riwaya zenyewe
viongozi na watu wetu. Ni dondoo linaloonyesha aina ya kuwezwa vibaya sana
ukilinganisha na zile siasa za miaka ya 1960 hadi 1970 zilizotupa tamaa ya kukwamuka
na kuwa na ufahari wa kuwa sisi ni watu pia.
3.4 Lugha ya Mchanganyondimi10
Gromov (2004:6) anapiga ndipo anaposema kwamba sifa moja muhimu ya riwaya hii
mpya ya Kiswahili ni ile ya mchanganyondimi. Lakini Gromov haishii hapo, anafafanua
mchanganyondimi kama unavyotumika katika riwaya hii kwa kuuita mchanganyondimi
wa mbambizoviraka11. Kwa mfano, hadithi ya Babu Alipofufuka inaanza kama hadithi ya
mzuka, kisha inaingia katika maelezo ya matukio ya uhalisia katika jiji mojawapo la nchi
za Kiafrika na baadaye inamwongoza msomaji katika ukweli wa kifantasia ambao umo
katika dunia nyingine. Tena tunaelezewa kuporomoka kwa Pate ya Al-ikishafi. Kisha
inakuja habari ya UKIMWI ikifuatiwa na uharibifu wa tabaka ozoni. Halafu tunakutana
na Visaasili vya Wagiriki na Mungu wao wa pwani, yaani Proteus ambaye anahusishwa
na utandawizi wenyewe au kiongozi mkuu wa nchi za Kiafrika ambaye anautumikia
utandawizi huku akienda dhidi ya nchi yake na watu wake.
Wamitila katika Bina-Adamu, pia anatumia mchanganyondimi usio mipaka ya
urejeleshi12 kuhusu ‘matokeo ya historia za dunia’, ‘fasihi’, mchanganyo wa ‘visaasili’,
‘matini za kidini’, ‘falsafa’ na mambo muhimu ya uhalisia wa maisha ya kisasa. Riwaya
hii pia inaingiza wababe kama Wotan, Pandora, Joseph Mengele, Emperor Hirohito, Che
Guevara na maandishi ya Heike Monogatari na William Dubois’ The Soul of Black Folk.
Katika riwaya mbili za Kezilahabi, Nagona na Mzingile kuna mchanganyondimi wa
aina hiyohiyo, ingawa kwa mtindo na nyenzo tofauti. Kwa mfano, matini inajengwa kwa
lugha faragha ya mwandishi mwenyewe anayejificha nyuma ya wahusika wake, lugha
ambayo imo katika mkondo simulizi, lakini kila mara inaingiliwa kati na miketo ya
kifilosofia, dini, saikolojia, maneno ya mitume waliofufuka na wahusika wengine wenye
uwezo wa kuishi maelfu ya miaka. Hivi ndivyo miketo hiyo inavyopachikwa
kimbambizoviraka juu ya matini kuu ya riwaya ya Nagona (uk.15):
Uwaonao katika duara hii ni kikundi kidogo tu cha waliokuwa wabishi katika usakaji wa
njia. Yule pale ni Plato, na yule ni Socrates. Huyu hapa ni Aristotle. Yule ni Hegel huyu
ni Darwin na waliokaribiana na Marx ni Freud na huyu ni Nietzsche ...
Na si kama wafu hawa wanatajwa majina tu – lakini pia wanaonyeshwa kushiriki
katika historia yao ya mapambano ya kifalfasa na kiitikadi kama pale tunapoambiwa:
[S]asa hivi wametulia kidogo. Zamani wakianza majadiliano na roho zao ilikuwa vurugu
tupu. Na wakianza majadiliano ya wao kwa wao basi hapo duara iliwaka moto ...(uk.15)
3.5 Lugha na Falsafa
Kwa kawaida matukio makuu yote yanayokuja kuwaelemea watu vibaya sana, huzusha
mijadala ya kifalsafa. Kuzuka kwa neno utandawazi na taathira ya neno hili katika
maisha ya watu katika ubinafsi wao, ujamii wao, utamaduni wao, imani zao za kijadi na
10 Tunalitumia neno hili kwa maana ya ‘collage’, yaani mbandikizo wa picha mbalimbali ambazo si lazima ziwe na
uhusiano wa moja kwa moja juu ya mji wa sanaa ya uandishi
11 Tunalitumia neno hili kwa maana ya ‘collage’, yaani mbandikizo wa picha mbalimbali ambazo si lazima ziwe na
uhusiano wa moja kwa moja juu ya mji wa sanaa ya uandishi
12 Tafsiri ya Allusion
kidini, kuwepo kwao duniani kiujumla, kuwepo kwao duniani kama kikundi cha watu wa
jinsi fulani, kuangamia kwao, mwelekeo wao wa maisha ya baadaye, utambulisho wao,
heshima yao kama binadamu ni mambo kadha ambayo bila ya shaka yanazua masuala ya
kifalsafa kama vile: nini mtu? Nini utu? Nini ubinadamu? Nini uraia? Nini uzalendo?
Nini ukweli na nini uwongo? Nini uhuru? Nini siasa? Ipi siasa bora? Nini historia? Nini
dini? Kwa nini mtu alazimishwe kugeuza imani yake? Kwa nini mtu alazimishwe kuishi
wanavyotaka watu wengine? Nini raha na furaha? Nini maendeleo? Haya ni baadhi ya
masuala machache yanayoulizwa katika riwaya hii ambayo inaweza ikaitwa riwaya ya
kisomi au kifalsafa. Kazi zote kwenye mkusanyiko wa riwaya hii, kwa namna fulani, zina
kipengele hiki muhimu cha usomi ambamo falsafa ya aina fulani inajadiliwa na
kuendelezwa au kuchokozwa.
Nagona inajishughulisha mno na suala la kutafuta ukweli. Safari yote ya mhusika
mkuu ‘mimi’ ni safari ya kuutafuta ukweli ambao unaonyeshwa katika riwaya hii una
nyuso nyingi. Mzingile inakita katika mzugiko wa akili wa mwanadamu katika kuumba
hofu kwa dhana (kwa mujibu wa mwandishi) yake mwenyewe – dhana ya Uungu – kwa
hivyo suala la nini dini? Nani Mungu? Ni dhana gani ya Uungu? Ina dhima gani dini
katika maendeleo ya mwanadamu?
Ziraili na Zirani inasaili haki ya dini moja kujiona bora kuliko nyingine iwapo lengo
hatimaye ni kumwabudu Mungu mmoja yuleyule. Kwa nini watu wanagombana na
kupigana katika vita vikali vya jihadi ikiwa ukweli wa Uungu ni mmoja na dini hatimaye
zinafanana sana? Aidha inalaumu uwezo wa Kiungu unaosababisha tofauti za kimaisha
hapa duniani. Kwa nini wengine wamepewa nafasi ya kuishi bora zaidi kuliko wengine
na Mungu wao ni yuleyule mmoja? Jambo hili limeleta kani ya kufanyika mapinduzi
mbinguni yakiongozwa na waasi akina Zirani, mhusika mkuu na wenzake wengine
wenye msimamo wa kimaendeleo.
Katika Babu Alipofufuka, Dunia Yao na hata Bina-Adamu, suala zima
linaloshughulikiwa kifalsafa ni siasa. Nini maana ya uongozi au uongozi bora? Nini
uhuru? Nini maendeleo? Nini maana ya kuishi? Nini uraia wa mtu? Nini uzalendo? Kwa
nini pesa ina nguvu zaidi kuliko kitu chochote –hata zaidi ya heshima ya mtu? Zaidi ya
mke na mtoto wake mtu? Zaidi ya hata nafsi yake mtu? Kwa nini kikundi kidogo cha
watu kipange maisha ya watu wengi katika jamii fulani na nje ya jamii hiyo? Kuna dunia
ngapi katika dunia moja ya jamii fulani? Mipaka ya dunia hizo ni miembamba au mipana
kiasi gani? Nini maana ya kifo? Nini maana ya kuishi? Inawezakana mtu ambaye anaishi
kuwa ameshakufa? Nguvu zipi zinaongoza ulimwengu wetu? Zinaongoza kwa masilahi
ya nani na kwa taathira gani? Katika Bina-Adamu (uk. 53) na riwaya nyingine nguvu hizi
zinaelezewa kwa ungamo la nguvu zenyewe zinazojieleza hivi:
[I]takuwa vigumu kupambana nami ... Nimewaingia akilini kabisa. Ninahisika kwingi
hata nisikokuwako. Kutokuwako kwangu ndiko hasa kuwako kwangu! ...
Mwandishi wa Bina-Adamu (uk.154-155) anafikia hata kupendekeza kwa maneno ya
wazi wazi namna gani ya kupambana na nguvu hii:
[J]amii inahitaji kuelimishwa upya kuanzia chini hadi juu, mtoto hadi mzee, wote ... e.e.
Huu ndio ukombozi ufaao; matakwa ya jamii yawekwe mbele. Kumbuka siku za
ukombozi kuletwa na mtu mmoja zimepita! ... Unganeni kiuchumi, kisiasa na kijamii.
Umoja ni nguvu! Mtaishia kumfunga yeyote, awe mkubwa! Nilikumbuka kile kisa cha
Gulliver; jitu kubwa lililoishia kufungwa na wale mbilikimo waliokuwa wakiitwa
Lilliputians ... Kwa njia hii mtaacha kuishi pembezoni pembezoni mwa kijiji! Itabidi
tuwe nguli kupambana na hasidi wa kijiji – Global villain.
3.6 Lugha na Mvunjiko wa Utambulisho
Uharibifu mmoja mkubwa sana wa utandawazi au bora tuseme utandawizi ni ule wa
nguvu zake za kuvunja na kuharibu utambulisho wa watu katika viwango mbalimbali:
kibinafsi, kinchi au taifa, kisiasa, kiuchumi, kijamii, kiutamaduni na kidini. Tunaambiwa
katika Bina-Adamu (148) ... [U]limwengu umekuwa kijiji kidogo siku hizi, mipaka haipo
tena ...
Mtu binafsi amevunjikavunjika kwa sababu hana pahala pa kusimama katika
kudai haki zake za msingi kama vile kuweza kupata kazi ya kumwendeshea maisha yake
kwa sababu utandawazi/utandawizi umevuka mipaka na kuvunja kuta kuchukua vyombo
vya taifa na kuvitia katika mitaji na utajiri au masilahi yao: viwanda vimenunuliwa, benki
zimechukuliwa, machimbo ya madini na rasilimali nyingine yamehodhiwa, vyombo vya
huduma vya wananchi kama mashirika ya usambazaji umeme vimebinafisishwa, huduma
za maji na mafuta na sehemu ya shule na hospitali hazimo tena mikononi mwa serikali za
wananchi. Uko wapi usalama wa taifa ukizingatia haya? Kinchi au kitaifa
utandawazi/utandawizi umevunja nguvu na uwezo wa maamuzi ya nchi kiuchumi na
kijamii. Nchi na taifa lazima zifuate masharti ya vyombo vinavyotetea utandawazi kama
vile WTO. Kwa maneno mengine nchi changa ambazo haziwezi kujitegemea, sio tu
hazina tena sauti katika mambo ya kiuchumi bali pia katika yale ya kisiasa na ya kidunia.
Ni ajabu, kwa mfano, kuona kwamba nchi za Kiafrika au Dunia ya Tatu hazina msimamo
wa dhahiri wa suala la ujangili na vita vinavyoendeshwa Iraki na Afghanistan –kimya
kimetawala katika nchi hizi ambazo miaka iliyopita zilikuwa mstari wa mbele kukemea
matendo ya mataifa makubwa. Ni muhimu kuwa na msimamo wa mambo haya kwa
sababu Waswahili husema ukimwona mwenzako ananyolewa na wewe tia maji.
Sikwambii tena kiutamaduni, nchi changa zimekuwa nchi pokezi za tamaduni za wenzetu
na hasa zile mbaya, hata maana ya utandawazi inageuka kuwa utanda-upande-mmoja.
Katika riwaya hii mpya, lugha inayotumika mara nyingi ni ile ya kutokuwa na
hakika tena ya jambo lolote. Hakuna hakika ya chakula, makazi, elimu, matibabu,
heshima ya mtu, heshima ya nchi, uraia wake mtu, heshima ya Uafrika ambayo tokea
mwanzo ilikuwa imekandamizwa sana wakati wa ukoloni. Mambo haya yote ndiyo
yaliyokuwa msingi uliofanya nchi za Kiafrika na Dunia ya Tatu kupigania uhuru. Jambo
hili limemfanya Wamitila kulalamika na kuhitimisha udhalimu wa utandawazi katika
Bina-Adamu (uk.137) kwa kusema:
[H]izi SAPS13 zinatusapa uhai ... Kijiji cha wizi hiki ... Dola inatukaba ... Yen ni kamba
ya kitanzi!
Ushahidi wa malalamiko haya umo pia katika Babu Alipofufuka (uk. 154) pale tunaposoma
kwenye mabango ya maandamano ya kupinga utandawizi:
... M’mezifisidi nafsi zetu ... M’meivunja heshima yetu ... Vijana wetu wanapotea ... Vifo vya
njaa na maradhi sababu si sisi ... Hatuna nafasi panapostahiki nafasi zetu ... Ardhi
inachukuliwa hivihivi tunaona ... Kesho yetu imo katika giza ... Tunaangamia ...
Tumeshakwenda kapa ...
13 Kwa urefu ni ‘Structural Adjustment Programmes’
Na hivi ndivyo tunavyomsikia mhusika mkuu Ndi-14 katika Dunia Yao (1) akilalama jinsi
alivyovunjika kibinafsi...
[L]abda nipo. Pengine sipo! Tofauti gani? Ndiyo, moyo bado unatuta. Hii labda ndiyo
ishara pekee iliyobaki. Pangaboi linapepea pasi na nguvu za umeme. Kishumaa kidunya
kinadiditia na kujitahidi kunilaza salama. Sijui lini lakini. Mwaka gani? Mwezi gani?
Siku gani? Saa? ... Wakati hauwaziki tena –mashiko hauna, mantiki umeachana –
umepoteza maana! Saa inatik’tika mezani. Inasonga mbele. Aaaa, saa! Chombo tu; na
nambari zake, ishara ya jinsi wakati unavyokupuka –kasi, kasi; kasi isiyo kizuwizi.
Lakini mbele nd’o wapi? Na nyuma ndiko kupi? N’navyojua mimi, wakati umeketi
kichwani. Si juu ya uso wa saa ...
3.7 Mbinu Lugha zenye Mnasaba na Utandawazi/Utandawizi
Kuna baadhi ya mbinu lugha ambazo waandishi wa riwaya hii wanazitumia kwa
makusudi kuonyesha tabia na taathira ya utandawazi kwa nchi zetu. Mbinu ya kwanza ni
ile ya maneno ambayo wameyaunda kuelezea hali hiyo. Kwa mfano, katika Babu
Alipofufuka tunakuta meneno ‘uleo-wa-mawazo’, ‘ndoto-macho’, ‘kurongofywa’,
‘ukofiwatu’, ‘mkonowazi’, ‘mwambangoma’, ‘asijeurike’, ‘nakuona-wewe-mimihunioni’,
‘umaitikwenenda’, ‘mfuhai’, ‘watengeza-utamaduni-mpya’, ‘zizikinyesi’,
‘wenyesingazao’, ‘kizamoto’, ‘n’kupande-n’kushuke-kasheshe’, ‘tumejitoa-tumejitiawasasa’,
‘wapenda furaha’, ‘wapendakachiri’, ‘mmezakaseti’, ‘bwana-mwenye-nyumbakubwa’
n.k.
Katika Dunia Yao tunasoma maneno kama vile: ‘pangaboi’, ‘mkaushausingizi’,
‘nyama- na- mifupa’, ‘kandamoyo’, ‘mtu- nyama– na- mifupa’, ‘baruapepe’,
‘wavumeme’, ‘umwamba- wa- kiume’, ‘kisichofaa- kinachofaa’, ‘babkubwa’,
‘elimujamii’, ‘wanaelimujamii’, ‘mkokota rikwama’, ‘dongo- la- zamani’, ‘mtapionuru’,
‘ki-TshombeTshombe’, ‘kimulatomulato’, ‘ki-hybridhybrid’, ‘ndoto-kweli’, ‘wauzatarabizuna-
na- uzuri’, ‘Superboyswawili’ n.k.
Katika Bina-Adamu, tunakutana na maneno kama ‘Bina-Adamu’, ‘wasichanawavulana’,
‘UMERO-JAPA’, ‘Zakongwe’, ‘Fyura’, ‘Fyuraha’, ‘rubo’, ‘Mefu’,
‘Yanguis’, ‘FUJO ASILIA’, ‘UMOJA WA FUJO’, ‘Jengo la Pembetano’, ‘zinatusapa’,
‘taifa-dola’, ‘Abubepar’, ‘Binberu’, ‘Mwajihawaa’, ‘Mwanakabila’, ‘Binrangi’,
‘Mkengeushi’ n.k.
Pia riwaya hii inaingiza kwa makusudi maneno mengi ya kigeni kusisitiza usomi wa
riwaya yenyewe na pia ugeni na wizi wa utandawazi wenyewe. Katika Nagona kwa
mfano, tunapata maneno kama ‘Ego’, ‘Id’, ‘Superego’, ‘Sphinx’, ‘Cogito’, ‘Causa’
‘Ultima’, ‘Disciplina Voluntatis’, ‘De Anima’, ‘Politica’, ‘Metaphysica’, ‘De Poetica’,
‘Totem’, ‘Oedipus Complex’, ‘Neurosis’, ‘ashab’, ‘tabilin’ na ‘tafsir’.
Katika Babu Alipofufuka tunaona maneno kama ‘Gangar Wa’azu’, ‘Doggy’, ‘Neo-
Casino’, ‘Proteus’, ‘Limonsin’, ‘shoyu’, ‘sake’, ‘beetles’, ‘spring chicken’, ‘semaa wa
twaa’, ‘FKK’, ‘CD-ROM’, ‘Mona Lisa’, ‘zerha’, ‘manekineko’.
Katika Dunia Yao tunapata maneno kama ‘Muse’, ‘CD’, ‘video’, ‘TV’, ‘taj’widi’,
‘maulidi’, ‘kasida’, ‘C Licence’, ‘TX’, ‘chip’, ‘Hillman’, ‘Vauxhall’, ‘mamluki’, ‘The
Aritos’, ‘New World Order’, ‘WTO’, ‘Globalisation’, ‘sanctions’, ‘RAP’, ‘Paradise’, ‘I
Need to Know’, ‘fantastic’, ‘Skyscrapers’, ‘cloning’, ‘dialectics’, ‘Zeus’, ‘Mnemosyne’,
14 Neno lenyewe kama jina la mhusika mkuu ‘Ndi-‘ limemeguka, limevunjika.
‘Calliope’, ‘Clio’, ‘Erat’o’, ‘Euterpe Melpomene’, ‘Polyhymnia’, ‘Terpsichore’, ‘Thalia’,
‘Urania’ n.k.
Katika kipengele hiki pia tunaingiza uvunjaji wa kanuni za kisarufi, kiutanzu na
kiujumi katika matini ya baadhi ya riwaya za mwelekeo huu. Uvunjaji huu
unalinganishwa na uvunjaji wa kanuni kadha katika jamii ambazo zilidhaniwa
zimeshakita na zisingeweza kuvunjwa kamwe. Ni wazi kwamba katika Babu Alipofufuka
na Dunia Yao kanuni za sarufi zinavunjwa makusudi kama tunavyoona katika Babu
Alipofufuka...[u]wanja-wa-ndege-wa-kimataifa alisimama kujitayarisha kwa ufunguzi wa
milango (uk.29) ... komputa alimwambia kwamba mkewe Bi. Kiluba alikuwa akimsubiri
kumbi la chini (uk.67). Au katika Bina-Adamu tunagundua kauli kama ...[I]nasemwa
kuwa ... (uk.35) ambayo imechukuliwa moja kwa moja kutokana na Kiingereza balada ya
Kiswahili Inasemekana kuwa ... [W]anaamini kwamba ukoo wao ni tukufu (uk.38) badala
ya Ukoo wao ni mtukufu ... [H]apana, labda ni kimo changu cha mtoto (uk.45) badala ya
Hapana, labda kimo changu cha utoto ...
Matumizi wa sanaahati15 – yaani namna ya kucheza na mwandiko wa maneno ili
kutoa hisia fulani ya kimaana au ujumi ni njia nyingine ya matumizi ya lugha kuelezea
hali na taathira za utandawizi katika baadhi ya riwaya hizi, hasa katika Babu Alipofufuka,
Dunia Yao na Bina-Adamu. Katika Babu Alipofufuka ukosefu wa uaminifu na kigeugeu
cha utandawazi wenyewe na viongozi wakuu wa nchi wanaoutekeleza kwa shauku,
unaelezewa katika mabadiliko ya uherufi katika sura mbalimbali kama vile tunavyoona
katika neno Proteus linavyochorwa kiwimawima, kimlalo (kiyombo), kimkolezo,
kimfifio, kiudogo na kiukubwa. Kwenye Dunia Yao tunapata nambari 36 ya miaka ya
uhuru wa Zanzibar inakolezwa makusudi ili msomaji atafakari mafanikio na
mashindikano ya wakati wa baada ya uhuru wa miaka hiyo 36. Maneno Wewe na mimi
(uk.20) yanatofautishwa kwa mkozesho na udogowesho kusisitiza ubinafsi na ule ukilamtu-
na-lake wa siku hizi. Usichochote nao unasisitizwa katika mpromoko wa maneno
cider na nonentity. Neno Superboyswawili linalosisitiza Umarekani na Urusi wakati wa
vita baridi linatiliwa mkazo na mkolezo wa wino. Neno ilhamu linalosisitiza kuzuka kwa
riwaya mpya katika wakati wa utandawazi na kuwepo mtindo wa riwaya ndani ya riwaya
(metafiction) au uzungumziaji wa riwaya ndani ya riwaya hasa kujibu hoja ya baadhi ya
wahakiki kwamba riwaya sharti ichukue mkondo wa uhalisia – limekozeshwa wino pia.
Bina-Adamu inatumia mkolezo wa wino au/na yombo na herufi kubwa katika msisitizo
wa baadhi ya maneno yake kama Njia ya UHALISIA, UMERO-JAPA, Gastarbeiter,
Nurenibaga, daktari wa kifo, Osagyefo n.k.
Muhimu sana katika mbinu hii ni jinsi inavyotofautisha sauti za wasimulizi na
wahusika mbalimbali katika riwaya ambamo herufi wima, herufi mlalo au yombo na
herufi yombo zilizokolezwa, zinatafautisha wasimulizi na wahusika mbalimbali katika
riwaya hii. Pia mbinu ya kuingiza mtindo wa utanzu mwingine katika utanzu wa riwaya
kama vile tunavyoona Kezilahabi anapojenga matini yenye mtiririko wa kitamthilia (wa
mazungumzo na majibu) katika sura 8 (uk. 47-52) yote inayojadili ufisadi, ngono na
ukandamizaji wa kisiasa ulivyotawala duniani. Pia mwandishi huyu anavyotumia
ufupisho wa sura yenyewe kama vile sura ya 10 (uk. 62) ambayo ina aya nne
ndogondogo tu. Kwa kweli, riwaya za Kezilahabi ni fupi mno, kwa kiasi cha Nagona
kuwa na kurasa 62 na Mzingile 70.
15 Tafsiri ya graphicart
Mbinu ya mkarara wa kauli na maneno teuzi ni muhimu pia katika matumizi ya
lugha –mbinu inayorejelea utandawazi/utandawizi na kusisitiza baadhi ya matokeo yake
ambayo msomaji anatakiwa ayape uzito katika kuyafikiri.
Katika Nagona maneno ‘ukweli’, ‘mshumaa’, ‘vichaa’, ‘vicheko’, ‘ungamo kuu’,
‘ukimya’, ‘njia’, ‘barabara’, ‘mto’, ‘paa’, ‘ndege’, ‘mti’, ‘msitu’, ‘milima’, ‘mabonde’,
‘duara’, ‘vitabu’, ‘ukosefu wa watu’, ‘paka’, ‘mkombozi’, ‘ajali’, ‘ndoto’,
‘maluweluwe’, ‘uta’ na ‘mshale’ ni maneno yanayorudiwarudiwa kila wakati.
Katika Mzingile ‘mwanga’, ‘karne’, ‘kichaa’, ‘mkombozi’, ‘safari’, ‘ndoto’, ‘mto’,
‘giza’, ‘mzee’ na ‘ukungu’ ni baadhi ya maneno yanayorejewa kila baada ya muda.
Katika Babu Alipofufuka maneno ‘Proteus’, ‘Limonsin’, ‘Doggy’, ‘mzuka’, ‘Neocasino’,
‘kimya’ na ‘kompyuta’ ni maneno yanayotajwa sana. Katika Bina-Adamu
maneno ‘Bina-Adamu’, ‘P.P’, ‘huntha’, ‘Wotan’, ‘mto’, ‘safari’, ‘njia’, ‘Fyura’,
‘Yanguis’, ‘utandawazi’, ‘global village’ na ‘wizi’ ndiyo yanayojitokeza sana.
Lakini mbali na neno moja moja, baadhi ya kauli au picha zinazojengwa kwa
maneno mengi ambazo hurudiwa tena na tena kama tunavyoona katika Babu Alipofufuka
(uk.92, 96) kauli ya La, hatutaki, hata ikiwaje hatulali tena... na katika Bina-Adamu
(uk.140, 148) picha ya kuwa Ulimwengu umekuwa kijiji kidogo siku hizi, mipaka haipo
tena ... inarudiwa tena na tena ingawa kwa maneno mengine. Kauli ya Hii ndiyo bustani
yao ya Eden inarejewa mara kadha (uk.64, 110). Pia katika kitabu hikihiki tunakuta kauli
Sio sisi tu akina Churchill, ukoo wa Kaiser, ukoo wa Gaulle, kina Franco na muhimu
zaidi P.P. anafanya hivyo! Huu ni ulimwengu wa uwongo... (uk.50, 51). Picha nyingine
zinazorudiwarudiwa katika riwaya hii ni ile ya hofu, ujinga, wizi, ufisadi, unanganyi na
unyang’anywaji.
4.0 Hitimisho
Mjadala tuliouendeleza katika makala haya unarejelea na kuthibitisha tasnifu maarufu
katika somo la fasihi; ile tasnifu inayosisitiza kwamba, kama maisha ya mwanadamu
mwenyewe, fasihi nayo lazima ibadilike hasa wakati wa matukio makuu ya kutisha au
kufurahisha kama utandawazi/utandawizi ambayo yanabadilisha kwa kiasi kikubwa,
maisha ya watu wa jamii fulani. Kwa sababu lugha ni nyenzo ya msingi ya kubunia na
kuwasilishia kazi ya fasihi, basi lugha haina budi kukidhi kimaumbo, kimiundo na kikazi,
mahitaji ya kazi ya fasihi na mahitaji ya jamii yenyewe inayobadilika.
Marejeo
Bertoncini, Elena. (2002): When Grandfather Came to Life Again – S. A. Mohamed’s New Novel
Beyond Realism – makala iliyotolewa kwenye Kongamano la Kiswahili, Bayreuth.
Dittemer, Clarissa. (2002/2003): Said Ahmed Mohameds “Babu Alipofufuka” ein magischrealistischer
Roman – Kazi Maalum kwa Somo la Riwaya Mpya ya Kiswahili, Sehemu
ya Fasihi za Kiafrika kwa Lugha za Kiafrika, Chuokikuu cha Bayreuth.
Gromov, M. D. (1998). Nagona and Mzingile – Novel, tale or Parabole? Katika Jarida la
‘Afrikanische Arbeitspapiere 55: Kiswahili Forum V’, uk.73-78.
____________. (2004). Post-modernistic Elements in Recent Kiswahili Novels. Katika ‘The
Nairobi Journal of Literature: The Journal of the Department of Literature, University of
Nairobi’, 2, uk.28-36.
International Labour Force and Information Group. 1998. An Alternative View of Globalisation,
ILRIG, Cape Town.
Jauch, Herbert (ed.). (2001). Playing the Globalisation Game: The Implications of Economic
Liberalisation for Namibia, Labour Resource and Research Institute (LaRRI) Windhoek.
Kezilahabi, E. (1990). Nagona. Dar-es-salaam University Press.
___________. (1990). Mzingile. Dar-es-salaam University Press.
Khamis, Said A.M. 1999. Defamiliarisation and Experimentation in the Kiswahili Novel: A Case
Study of Kezilahabi’s Novel: Nagona. Hotuba isiyochapishwa ya kupokea uprofesa Chuo
Kikuu cha Bayreuth (Inaugural lecture).
________________. (2001). Fabulation and Politics of the 90s in Kezilahabi’s Nagona. Katika
Toleo la ‘African Languages Literature in the Political Context of the 1990s’. Bayreuth
African Studies 56 (2001): 119-133.
________________. (2003). Fragmentation, Orality and Magic Realism in Kezilahabi’s Novel:
Nagona. Katika ‘Nordic Journal of African Studies’ 12(1), uk.78-91.
King’ei, Kitula. (2002). Fantasy and Realism in the Modern Kiswahili Novel: A Critical Look at
Babu Alipofufuka by Said A. Mohamed – an unpublished literary review.
Mkangi, Katama. (1995). Walenisi. East African Educational Publishers: Nairobi.
Mkufya, W.E. (1999). Ziraili na Zirani. Hekima Publishers: Dar-es-salaam.
Mohamed, Said A. (2001). Babu Alipofufuka. Jomo Kenyatta Foundation: Nairobi.
______________. (2005). Dunia Y ao (kitatolewa na Oxford University Press: Nairobi).
_____________. (2005/2006). Mkamandume (kitatolewa na Longhorn (K) Ltd: Nairobi).
Murray, A. 2000. Public Sector Restructuring in Namibia – Commercialisation, Privatisation and
Outsourcing: Implication for Organised Labour, LaRRI, Windhoek.
Nicol Bran (ed.) (2002). Postmodernism and the Contemporary Novel: A Reader, Edinburgh
University Press.
Offiong, Daniel A. (2001). Globalisation: Post-Neodependency and Poverty in Africa, Fourth
Dimension Publishing Co.: Enugu Nigeria.
Rettová Alena. 2004. Afrophone Philosophies: Possibilities and Practice – The Reflexion of
Philosophical Influences in Euphrase Kezilahabi’s Nagona and Mzingile. Katika Jarida la
‘Kiswahili Forum’ 11, uk. 45-68.
Robert, Shaaban. (1951). Kusadikika. Nelson: London.
_____________. (1967). Kufikirika. East African Literature Bureau: Nairobi.
Ruigrok W & R van Tulder. 1995. The Logic of International Restructuring, Routledge:
London/New York.
Topan, Farouk, (2002). Babu Alipofufuka by Said A. Mohamed – an unpublished literary review.
Wamitila, K.W. (1991). Nagona and Mzingile: Kezilahabi’s Metaphysics. Katika Jarida la
Kiswahili 54 la (TUKI), Chuokikuu cha Dar-es-salaam, uk. 62-67.
____________. (1997). Contemptus Mundi and Carpe Diem Motifs in Kezilahabi’s Works.
Katika Jarida la Kiswahili 60 la (TUKI), Chuokikuu cha Dar-es-salaam, uk. 15-24.
____________. (2002). Bina-Adamu. Phoenix Publishers, Nairobi.
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
No comments:
Post a Comment